Saumu za Sunna


Maana ya saumu za sunna

Saumu za Sunna
Saumu yoyote amabayo sio ya lazima na mtu anaifunga ili kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu U
Na saumu ya sunna ina fadhila kubwa na malipo makubwa. Katika Hadithi Al-Qudsy kutoka kwa Abu Hureirah t Anasema: Amesema Mtume (saw): “Kila kitendo chema cha mwanadamu malipo yake huongezwa, jema moja hulipwa kwa kumi mfano wake mpaka kufikia mara sabini. Anasema Mwenyezi Mungu Mtukufu: Isipokuwa saumu, kwani hiyo ni yangu mimi, na mimi ndiye mwenye kuilipa” [Imepokewa na Bukhari na Muslim.].

Siku ambazo kwamba ni sunna kufunga.

1. Siku sita katika mwezi wa Shawwaal (Mfungo mosi)

Kwa kauli ya Mtume (saw): (Atakayefunga Ramadhani, kisha akafuatiliza kwa kufunga siku sita za Shawwaal, itakuwa ni kama aliyefunga mwaka mzima) [Imepokewa na Muslim.].
Sawasawa awe amezifunga siku sita hizi kwa pamoja kufuatana au siku mbalimbali zisizofuatana.

2. Kufunga Siku Tisa za Mwanzo wa Mwezi wa Dhulhijjah. (Mfungo tatu)

Kwa kauli ya Mtume (saw): (Hakuna masiku ambayo matendo mema ni bora zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu kuliko masiku haya – yaani masiku kumi ya Dhulhijjah – wakasema (maswahaba): hata jihadi kwa njia ya Mwenyezi Mungu? Akema (Mtume): “Hata jihadi kwa njia ya Mwenyezi Mungu, isipokuwa mtu aliyetoka (kwenda jihadi) yeye mwenyewe na mali yake, wala asirudi na chochote (yaani akafa vitani)” [Imepokewa na Bukhari.].
Na masiku haya yakatiliwa nguvu zaidi na siku ya A’rafa kando na hajj – nayo ni siku ya tisa ya mwezi wa Dhulhijjah; kwa kauli ya Mtume (saw): (Kufunga siku ya A’rafa nataraji kwa Mwenyezi Mungu kusamehewa mtu madhambi ya mwaka kabla yake, na mwaka uliyo baada yake) [Imepokewa na Muslim.].

3. Kufunga siku ya A’shuura na siku iliyo kabla yake.

A’shuura
Ni siku ya kumi katika mwezi wa Muharam (Mfungo nne).
Kwa kauli ya Mtume (saw): (Na kufunga siku ya A’shuura nataraji kwa Mwenyezi Mungu kusamehewa kwa mtu madhambi ya mwaka uliyo kabla yake) [ Imepokewa na Muslim.].
Na sababu ya kufunga siku hii ni kama ilivyothibiti kutoka kwa Abdillahi ibn Abbas anasema: (Aliingia Madina Mtume (saw) akawaona Mayahudi wamefunga siku ya A’shuura, akasema Mtume: Ni nini hiki (mnachofanya)? Wakasema: Hii ni siku njema, siku hii ndiyo siku Mwenyezi Mungu aliyowaokoa wana israili kutokamana na maadui zao, basi akaifunga siku hii Nabii Musa. Akasema Mtume: Basi mimi nina haki zaidi kwa Musa kuliko nyinyi, akaifunga Mtume siku hiyo na akaamrisha watu kuifunga) [Imepokewa na Bukhari.].
Na inapendekezwa vile vile kufunga siku ya tisa, kwa ilivyo pokelewa kutoka kwa Mtume (saw) Alisema (Lau nitaishi mpaka Mwaka ujao nitafunga siku ya tisa) [ Imepokewa na Muslim.]

4. Kufunga Masiku meupe ya kila mwezi

Masiku meupe
Nayo ni tarehe kumi na tatu, na kumi na nne, na kumi na tano ya kila mwezi katika miezi ya kiislamu, na yameitwa meupe; kwasababu usiku wa masiku haya hunga’ra kwa mwangaza wa mwezi.
Kama ilivyothibiti kutoka kwa AbdulMalik ibn Minhal kutoka kwa babake: Kwamba (babake) alikuwa pamoja na Mtume (saw) akasema (kumwambia mwanaye – AbdulMalik): Alikuwa Mtume (saw) akiwaamrisha kufunga masiku meupe, na akisema: (Masiku) haya ni saumu za mwaka) [Imepokewa na Ibnu Hibbaan.]

5. kufunga siku mbili – jumatatu na alhamisi katika kila wiki.

Kama ilivyopokewa kutoka kwa Abu Hureira t kwamba Mtume ﷺ amesema: “Hupandishwa matendo (juu kwenda mbinguni) kila jumatatu na alhamisi, basi napenda matendo yangu yapandishwe hali ya kuwa nimefunga” [Imepokewa na Tirmidhi.].

6. Kufunga siku Moja na kula siku Nyingine

Bora katika funga za sunnah ni saumu ya Nabii Daud juu yake iwe amani – Alikuwa akifunga siku moja na kuacha siku moja; kutoka kwa Abdillahi ibn A’mru t Anasema: Amesema Mtume (saw): (Hakika saumu ya kupendeza sana mbele ya Mwenyezi Mungu ni saumu ya Daud, na alikuwa akifunga siku moja na kula siku moja) [Imepokewa na Nasaai.].

Comments

Popular Posts